MFUMUKO WA BEI UMESHUKA
Dar es Salaam. Mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia Desemba mwaka jana umeshuka hadi kufikia asilimia 4.8 kutoka asilimia 5.8 ya Novemba kutokana na kupungua kwa bei za bidhaa mbalimbali ikielezwa kwamba kupungua huko kulikuwa hakujatokea kwa miaka miwili iliyopita.
Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii,
Ephraim Kwesigabo aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa kushuka huko
kumetokana na kupungua kwa kasi ya upandaji bei ya bidhaa na huduma
ikilinganishwa na ilivyokuwa Novemba.
Alisema mfumuko wa bei za vyakula na vinywaji
umepungua hadi asilimia 5.7 Desemba kutoka asilimia saba ya mwezi
uliokuwa umetangulia.
Alitaja baadhi ya vyakula vilivyochangia kushusha
mfumuko huo kuwa ni mahindi yaliyoshuka kwa asilimia 11.3, unga wa
mahindi (7.6), samaki (4.0), ndizi za kupika (3.2), mbogamboga kama
kabeji (11.5), muhogo (10.5) na sukari iliyoshuka kwa asilimia 4.2.
Bidhaa zisizo za chakula nazo zilipungua. Mafuta
ya taa yalishuka kwa asilimia 5.4, dizeli (7.5), petroli (3.1) na simu
za mkononi zilishuka kwa asilimia 2.8.
Takwimu hizo mpya zinaonyesha kuwa fahirisi za bei
zimeongezeka kutoka 144.02, Desemba mwaka 2013 hadi kufikia 150.92
Desemba mwaka jana.
Hata hivyo, mfumuko wa bei unaopimwa kwa kipimo
cha mwezi hadi mwezi umeongezeka kidogo kwa asilimia 0.2 ikilinganishwa
na ongezeko la 0.6 Novemba, 2014.
Wastani wa mfumuko wa bei 2014
Mbali na mafanikio hayo, Kwesigabo alisema wastani
wa mfumuko wa bei wa Taifa kuanzia Januari hadi Desemba, 2014 ulishuka
kwa asilimia 1.8 kutoka asilimia 7.9 mwaka 2013.
“Mfumuko wa bei wa Taifa ulikuwa na mwenendo imara
kwa kipindi chote cha mwaka 2014 na kiwango cha chini kabisa kilikuwa
asilimia 4.8 Desemba wakati cha juu kabisa kilikuwa asilimia 6, 7
Agosti,” alisema.
Meneja wa Utafiti wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT),
Johnson Nyella alisema kuwa mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia Desemba,
umefikia mahali pazuri kiasi cha kuzidi kiwango cha malengo ya muda
mrefu ya asilimia tano.
“Tunatumaini mfumuko wa bei utaendelea kuwa nafuu
kipindi cha miezi ya hivi karibuni kwa kuwa hakuna viashiria
vinavyotishia bei kupanda.
No comments:
Post a Comment